Maumivu ya kiuno
From Wikipedia, the free encyclopedia
Maumivu ya kiuno (kwa Kiingereza: lumbago) ni hali inayotokea mara nyingi na inayohusu misuli na mifupa ya upande wa chini wa mgongo. Hali hii huathiri takriban 40% ya watu kwa wakati fulani maishani mwao.
Maumivu ya kiuno ni tatizo la kawaida na lenye gharama. Mchoro unaonyesha eneo la kiuno katika kiunzi cha mifupa cha binadamu. | |
ICD-10 | M54.5 |
---|---|
ICD-9 | 724.2 |
MedlinePlus | 007422 Kigezo:MedlinePlus2 |
eMedicine | pmr/73 |
MeSH | D017116 |
Maumivu ya kiuno yanaweza kuainishwa kwa urefu kama maumivu makali ya ghafla (yanayodumu kwa kipindi cha chini ya wiki 6), maumivu sugu ya wastani (wiki 6 hadi 12), au maumivu sugu (zaidi ya wiki 12). Hali hii pia inaweza kuainishwa kulingana na visababishi kama inasababishwa na jeraha au sivyo au maumivu hame.
Katika visa vingi vya maumivu ya kiuno, kisababishi kikuu maalumu hakitambuliwi wala kukisiwa, kwa kuwa maumivu huaminika kutokana na jeraha kama vile mkazo wa misuli au mkazo wa viunga. Ikiwa maumivu hayaponi baada ya kutibiwa kwa njia isiyohusisha upasuaji au ikiwa maumivu yataandamana na "tahadhari" kama vile kupungua uzito bila sababu, homa, au matatizo makuu ya kihisia au mwendo, uchunguzi zaidi unaweza kuhitajika kubaini kisababishi kikuu.
Mara nyingi, vifaa vya utambuzi kama vile tomografia iliyohasibiwa kwa eksirei havihitajiki navyo huandamana na hatari zake. Licha ya athari hizi, matumizi ya pichatiba kuchunguza maumivu ya kiuno yameongezeka.
Baadhi ya maumivu ya kiuno husababishwa na kuharibika kwa diski za baina ya pingili za uti wa mgongo, na uchunguzi wa kunyoosha mguu ni muhimu katika kubaini visa hivyo.
Katika watu wenye maumivu sugu, mfumo wa mwili unaochakata maumivu unaweza kutofanya kazi vyema, hivyo kusababisha maumivu makali ukijaribu kujibiza shughuli zisizo na hatari kubwa.
Matibabu ya maumivu ya ghafla ya kiuno kwa kawaida huwa haihusishi upasuaji, kama vile vituliza maumivu na kuendeleza kazi za kawaida jinsi mtu anavyoweza licha ya maumivu. Matibabu hupendekezwa kwa kipindi ambapo yanamsaidia mtu, huku dawa aina ya acetaminophen (inayojulikana pia kama paracetamol) ni ya kwanza kupendekezwa. Dalili za maumivu ya kiuno hufifia baada ya wiki chache, huku 40 - 90% ya watu wakipata nafuu kabisa baada ya wiki sita.
Kuna njia nyingi mbadala katika watu wasiopata nafuu baada ya matibabu ya kawaida. Opioidi zinaweza kusaidia ikiwa vituliza maumivu vya kawaida havitafaulu, ingawa kwa jumla hazipendekezwi kwa sababu zina madhara, hasa uraibu. Upasuaji unaweza kuwafaidisha watu wenye matatizo ya maumivu sugu na ulemavu unaohusiana na diski.Upasuaji pia unaweza kuwafaidisha watu wenye stenosisi ya uti wa mgongo. Hakuna manufaa bayana ya upasuaji yaliyopatikana kwa visa vingine vya maumivu ya kiuno yasiyo na kisababishi cha moja kwa moja.
Isitoshe, kuna matibabu ya dawa mbadala, ambayo ni pamoja na mbinu ya Alexander na mitishamba, lakini hakuna ushahidi wa kutosha kupendekeza matibabu hayo kikamilifu. Ushahidi wa utunzaji wa tibamwili na kunyooshaji uti wa mgongo umekumbwa na utata.
Maumivu ya kiuno mara nyingi huathiri hisia, tatizo linaloweza kuimarishwa kupitia ushauri wa kisaikolojia na/au dawa za kushusha utendakazi.