Karamu ya mwisho
From Wikipedia, the free encyclopedia
Karamu ya mwisho inamaanisha mlo wa mwisho wa Yesu Kristo hapa duniani, ambao aliula pamoja na mitume wake kabla hajakamatwa na hatimaye kusulubiwa.[1]
Katika Injili, hasa ile ya Luka, Yesu alishiriki mara nyingi karamu alizoandaliwa au alipoalikwa, kama vile ile ya arusi ya Kana. Ingawa jambo hilo lilisababisha aitwe "mlafi na mlevi", kwake ilikuwa nafasi ya kuzidi kujitambulisha kwa matendo na maneno na ya kutoa mafundisho yake.
Habari za karamu ya mwisho zinasimuliwa kirefu zaidi, hasa kwa sababu ndiyo wakati wa Yesu kuweka ukumbusho wake wa kudumu katika sakramenti ya mwili na damu yake.[2]
Wakristo wanafanya ukumbusho huo mara nyingi, lakini hasa Alhamisi Kuu.[3]
Barua ya kwanza kwa Wakorintho ndiyo ushahidi wa zamani zaidi kuhusu ibada hiyo. Baada yake Injili Ndugu pia ziliripoti matendo na maneno ya Yesu juu ya mkate na divai.
Injili ya Yohane haisimulii ekaristi ilivyowekwa, ila katika sura ya 6 inaripoti maneno mazito ya Yesu kuhusu mkate wa uzima, halafu katika karamu ya mwisho, pamoja na mengine, inaeleza Yesu alivyowaosha miguu Mitume na kuwaachia amri mpya ya kupendana kama yeye alivyowapenda, ambayo ndiyo lengo la ekaristi.[4][5][6]