![cover image](https://wikiwandv2-19431.kxcdn.com/_next/image?url=https://upload.wikimedia.org/wikipedia/commons/thumb/7/7c/Flag_of_the_Congo_Free_State.svg/langsw-640px-Flag_of_the_Congo_Free_State.svg.png&w=640&q=50)
Dola Huru la Kongo
From Wikipedia, the free encyclopedia
Dola Huru la Kongo (kwa Kifaransa: État indépendant du Congo, kwa Kiingereza: Congo Free State) lilikuwa jina la koloni kubwa katika Afrika ya Kati kutoka mwaka 1885 hadi 1908 na kitangulizi cha Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ya leo. Ilikuwa inamilikiwa kibinafsi na mfalme Leopold II wa Ubelgiji ilhali haikuwa chini ya serikali ya Ubelgiji.
![Thumb image](http://upload.wikimedia.org/wikipedia/commons/thumb/7/7c/Flag_of_the_Congo_Free_State.svg/640px-Flag_of_the_Congo_Free_State.svg.png)
![Thumb image](http://upload.wikimedia.org/wikipedia/commons/thumb/0/0b/Kongovrijstaat.jpg/320px-Kongovrijstaat.jpg)
![Thumb image](http://upload.wikimedia.org/wikipedia/commons/thumb/3/39/Leopold_ii_garter_knight.jpg/640px-Leopold_ii_garter_knight.jpg)
![Thumb image](http://upload.wikimedia.org/wikipedia/commons/thumb/5/52/MutilatedChildrenFromCongo.jpg/640px-MutilatedChildrenFromCongo.jpg)
Leopold aliweza kujipatia utawala juu ya eneo hilo kwa kushawishi mataifa mengine ya Ulaya kwenye Mkutano wa Berlin wa 1885 juu ya Afrika kwamba alikuwa akihusika katika kazi ya uhisani na hakutaka kukusanya ushuru wa biashara. [1] Kupitia Ushirika wa Kimataifa wa Kongo (International Association of the Congo) aliweza kueneza madai yake juu ya sehemu kubwa ya Beseni la Kongo.
Tarehe 29 Mei 1885, baada ya Mkutano wa Berlin kufungwa, mfalme alitangaza kwamba alikuwa na mpango wa kuendeleza mradi wake kwa jina la Dola Huru la Kongo (Congo Free State), jina ambalo lilikuwa bado halijatumika katika Mkutano wa Berlin na ambalo lilichukua rasmi nafasi ya "Ushirika wa Kimataifa wa Kongo" mnamo 1 Agosti 1885. [2] [3] [4]
Dola Huru la Kongo liliendelea kisheria kama nchi tofauti na Ubelgiji, chini ya utawala binafsi wa Leopold II, ingawa hakutembelea dola lake kamwe. [5]
Dola hilo lilijumuisha eneo lote la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ya leo kutoka 1885 hadi 1908, wakati serikali ya Ubelgiji ilipochukua utawala juu yake badala ya mfalme. [6]
Utawala wa Leopold huko Kongo mwishowe ulipata sifa mbaya kwa sababu ya ukatili uliofanywa dhidi ya wenyeji. Dola la Leopold II lilivuna pembe za ndovu, mpira na madini katika bonde la juu la mto Kongo na kuviuza kwenye soko la Dunia kupitia makampuni ya kimataifa, ingawa kusudi lake kuu lilikuwa kuinua wenyeji na kuendeleza eneo hilo. Faida za kiuchumi zilipatikana kwa njia ya kazi ya kulazimishwa iliyopatikana kwa kutumia matishio na adhabu kali pamoja na kuua watu na kusababisha vifo kwa njaa.
Chini ya utawala wa Leopold II, Dola Huru la Kongo likawa moja ya kashfa kubwa zaidi za kimataifa kwenye mwanzo wa karne ya 20. Taarifa ya balozi mdogo wa Uingereza Roger Casement ilisababisha kukamatwa na kuadhibiwa kwa maafisa ambao walikuwa wamehusika na mauaji wakati wa kampeni ya kukusanya mpira mnamo 1903. [7]
Upotevu wa maisha na ukatili ulikuwa mandharinyuma ya riwaya mashuhuri ya "Heart_of_Darkness" ya Joseph Conrad. Kitabu chake pamoja na taarifa za magazeti na za wamisionari vilisababisha kilio cha kimataifa.
Wataalamu wanaendelea kujadiliana kuhusu idadi ya vifo katika kipindi hicho. [8] Makadirio ya juu zaidi yanasema kuwa mfumo wa kazi ya kulazimishwa ulisababisha moja kwa moja au kwa njia nyingine vifo vya asilimia 50 ya idadi ya watu katika koloni. [9] Inaaminiwa kwamba sehemu ya vifo zilisababishwa na ukatili wa maafisa ya koloni na sehemu nyingine pia na magonjwa mapya yaliyoletwa na Wazungu ambayo wenyeji walikosa bado kinga yake.
Wapinzani na wakosoaji wa hali ya Kongo waliendesha kampeni kubwa katika Ulaya na Marekani iliyosambaza habari ya matendo ya kinyama yaliyotokea. Mwandishi mwingine aliyesaidia sana kufichua mabaya alikuwa Arthur Conan Doyle, ambaye kitabu chake The Crime of the Congo kilisomwa sana kwenye mwanzo wa karne ya 20.
Kufikia mwaka wa 1908, shinikizo la umma na ujanja wa kidiplomasia ulisababisha kukomeshwa kwa utawala wa Leopold II katika Kongo. Makampuni makubwa yalishawishi pia serikali ya Ubelgiji kubadilisha utawala kwa sababu walitaka kuwekeza katika sekta ya migodi iliyolala tu wakati ule.
Hivyo Bunge la Ubelgiji lilitoa sheria iliyoweka utawala wa nchi katika mikono ya serikali.
Nchi ilijulikana baadaye kuwa Kongo ya Kibelgiji. Kwa kuongezea, kampuni kadhaa kuu za uwekezaji wa Ubelgiji zilishinikiza serikali ya Ubelgiji kuchukua Kongo na kuendeleza sekta ya madini kwani ilikuwa karibu haijashughulikiwa. [10]