Wangulu (au Wanguu) ni kabila la watu wa Tanzania wanaoishi mipakani mwa mikoa minne ya Tanga, Dodoma, Manyara na Morogoro, hasa upande wa Kusini-Magharibi mwa mkoa wa Tanga ambako sasa ni wilaya ya Kilindi na upande wa Kaskazini-Mashariki mwa mkoa wa Morogoro ambako sasa ni wilaya ya Mvomero na milima ya Nguu. Upande wa Magharibi ni mkoa wa Manyara ambayo sasa ni wilaya ya Kiteto.

Masimulizi ya kale ya Mbega na Kimweri yanasema kuwa kabila la Wanguu ndilo kabila mama la makabila ya Wazigua, Wabondei, Wasambaa, Waluvu na Wakilindi, ambapo makabila hayo yanaendeleza mila na desturi za asili moja na katika umoja huo hujulikana pia kwa jina moja la Waseuta. Kwa asili Wanguu ni wafugaji na wakulima.

Mwaka 2009 walikuwa 219,000 hivi.

Utamaduni

Wanguu wana ngoma zaidi ya nne lakini iliyo maarufu ni sero kwa ajili ya kumtoa msichana aliye tayari kuolewa ambaye huitwa mwali; ngoma hiyo huchezwa siku 30 baada ya msichana kukaa ndani bila kutoka, mchezaji wa ngoma ya sero huvaa manyoya ya mnyama aitwaye mbega mabegani, kichwani na kiunoni, pia huvaa kengele nyingi miguuni na huwa na filimbi. Mwali huacha matiti wazi na huvaa kama mcheza ngoma na hucheza huku akitunzwa vitu mbalimbali. [1]

Majina

Majina ya Wanguu/Wangulu huanza na sa kwa mwanamume na ma kwa mwanamke yakiwakilisha koo zao ambazo hubebwa na wanawake, mwanamke anapozaa mtoto wa kiume, huyo ndiye huwa mkubwa wa ukoo, na koo zao ziko nyingi sana lakini maarufu ni Samnimbo, Samnapeho na kwa wanawake huitwa Mamnimbo au Mnapeho.

Utaalamu

Wanguu kwa miaka mingi na kwa kificho wamekuwa wakirithisishana utaalamu wa kutengeneza bunduki ambayo huiita gobole, kwa ajili ya woga kwa serikali wamekuwa wakitengeneza kwa siri kwa miaka mingi na hasa wanguu waishio milima ya unguu, utaalamu huo wamekuwa wakirithishana hadi sasa.

Ungulu na chanzo cha ukoloni

Eeno la Wangulu lilijulikana kwa jina ya "Nguru / Ngulu au kama inavyojulikana kwa siku hizi Nguu" kwa Wajerumani wakati wa ukoloni.

Ndiko mkoloni Mjerumani Karl Peters alifanya mkataba wa kwanza kwa maeneo yaliyokuwa baadaye koloni la Afrika ya Mashariki ya Kijerumani. Peters aliyekuwa ameondoka Saadani, alifika Nguru 23 Novemba 1884 [2] alipokutana na mmoja Masungu [3] Biniani.

Kufuatana na maelezo ya Peters, huyu alikuwa "Sultani wa Nguru" aliyefanya urafiki naye, baadaye aliweka alama yake kwenye karatasi iliyoandikwa na Peters na wenzake. Katika matini iliyopelekwa baadaye Berlin, mji mkuu wa Ujerumani, Masungu Binani kama Bwana wa "nchi za Katungekaniani na Kwindokaniani katika Nguru" alikubali kukabidhi haki zote za kiutawala na wa kiuchumi kwa Shirika la Ukoloni wa Kijerumani lililowakilishwa na Peters.

Kuna wasiwasi mwingi kama huyu Biniani alikuwa chifu au sultani wa eneo gani, pia kuna mashaka kama alielewa walau punje karatasi ilisema nini na kama alama ni kweli yake.

Hivyo ndivyo pia kuhusu "mikataba" mingine ya Peters. Lakini karatasi hizo zilitosha kuweka msingi kwa ukoloni wa baadaye.

Tanbihi

Wikiwand in your browser!

Seamless Wikipedia browsing. On steroids.

Every time you click a link to Wikipedia, Wiktionary or Wikiquote in your browser's search results, it will show the modern Wikiwand interface.

Wikiwand extension is a five stars, simple, with minimum permission required to keep your browsing private, safe and transparent.