Mabata bukini ni ndege wakubwa wa maji wa familia ya Anatidae. Wanaainishwa katika nusufamiliaAnserinae pamoja na mabata-maji. Mabata bukini ni ndege wakubwa sana lakini wadogo kuliko mabata-maji. Wana domo pana pia lakini shingo yao ni fupi zaidi. Wana rangi mbalimbali kama kahawia, nyeupe na nyeusi kadiri ya spishi. Hula mimea na pengine wadudu na nyungunyungu. Wanaweza kuwa wasumbufu wakiingia mashamba. Tago lao limejengwa kwa vijiti, manyasi n.k. karibu na maji na limetandikika na manyoya mororo.
Maelezo zaidi Uainishaji wa kisayansi, Ngazi za chini ...
Ndege hawa huzaana kwa kanda za kaskazini kabisa za dunia au juu sana ya milima. Spishi moja tu, Cereopsis novaehollandiae, huzaa katika nusudunia ya kusini na inaainishwa pengine katika nusufamilia yake binafsi. Wakati wa majira ya baridi mabata bukini huhama kanda za moto zaidi. Bata bukini hufugwa mahali pengi pa Afrika, lakini ndege mwitu hutokea tu kwa idadi kubwa huko Maroko, Aljeria na Tunesia wakati wa majira ya baridi ya Ulaya. Ndege wanaofugwa katika Afrika kusini kwa Sahara wanatokana aghalabu na bata bukini wa Uchina. Aina kadhaa zinatoka uzalishaji mtambuka wa mabata bukini wa Ulaya na Uchina.